safari ya mashaka
Hii ni simulizi ya Kijana mmoja ambaye anajulikana kwa jina la FRANK
Imesimuliwa na Frank, na Imeandikwa na Saidi R Bunduki
Leo katika kipindi chetu cha sitosahau anashea nasi historia yake ya kutoka Dar mpaka Mbeya kwa mguu safari ambayo ilidumu ndani ya siku takriban 6.
Frank ni kijana mwenye umri wa Miaka 28 kwa sasa ni dereva wa bajaji katika jiji la Mbeya. Mnamo mwaka 2014 alishauriwa na rafiki yake ambaye hakupenda jina lake tulitaje.
Rafiki yake huyu alikuwa ni Dereva wa daladala katika jiji la Dar es salaam. Aliambiwa na rafiki yake kuwa aende Jijini Dar ili akamtafutie kazi katika Kampuni ambayo alikuwa akifanyia kazi.
Frank aliamua kukubaliana na ushauri wa rafiki yake na siku ya safari ilipofika alisafiri kwa magari ya mizigo ambayo yalikuwa yakitoka Zambia kuelekea Dar es Salaam. Frank wakati huo hakuwa na kazi yoyote ndio maana aliamua kuenda Dar kutafutiwa kazi na rafiki yake ambaye walipotezana kwa takriban miaka minne.
Frank hakuwahi kufika Dar hivyo alielekezwa na rafki yake kuwa akifika dar amtafute ili aje amchukue kwakuwa wote walikuwa na mawasiliano haikuwa tatizo.
Gari ilifika Dar siku ya pili usiku. Kama tujuavyo kuwa watu wa magari makubwa wakati mwingine huwa hawana haraka hasa pale ambapo wanakuwa wameshasafirisha mzigo wao na wakiwa wanarudi. Frank alipofika Morogoro aliampigia simu rafiki yake yule ili kumfahamisha kuwa amefika Morogoro.
Lakini kwa bahati mbaya simu haikuwa hewani na kadiri alipokaribia ndipo alizidi kumtafuta best yake lakini juhudi zake ziligonga mwamba. Hatimaye mishale ya saa 4 usiku alifika katika jiji la Dar na kuachwa maeneo ya Mwenge ambapo watu wa gari waliendelea na safari yao. Frank akiwa hajui pa kuelekea na huku simu ya rafiki yake ikiwa haipatikani, alianza kuzurura usiku akiwa amechanganyikiwa na hajui wapi anaelekea.
Ghafla defender ya polisi ilipiga breki za nguvu nyuma yake karibu na kikundi cha wahuni ambao walikuwa wakicheza kamari. Jamaa wale walitimkana na kukimbia sehemu tofauti. Wakati Frank akishangaa huku na huko anakuja kushituka ameshachezea teke la ambalo lilimpeleka mpaka chini.
Baada ya kugundua kuwa wale walikuwa ni polisi wakifanya patrol usiku ule, naye aliamua kuungana na masela ambao walikuwa wanakimbia ovyo kuepuka kukamatwa na kupelekwa polisi. Lakini pale aliangusha simu na iliangukia kwenye mtaro na hakuweza kuiona tena na kuamua kukimbia kujinusuru uhai wake.
Baada ya purukushani zile kuisha, baadhi ya vijana walikamatwa na kupelekwa kunakohusika. Frank alijisachi mfukoni, pesa yake ya akiba shilingi elfu tano ilikuwepo, lakini simu ambayo aliishika mkononi akijaribu kumtafuta rafiki yake mara kwa mara hakuwa nayo kwani ilisha dondoka. Hapo alizidi kuchanganyikiwa ukijumlisha na maumivu ya kupigwa aliyokuwa nayo.
Kulipo pambazuka asubuhi, Frank hakuwa akijua yupo maeneo gani na hakujua atampataje rafiki yake. Lakini kwa bahati nzuri namba ya best yake alikuwa ameihifadhi kwenye karatasi ambayo ilikuwa katika mfuko wake wa suruali.
Aliomba simu kwa msamaria mwema mmoja na kumueleza shida yake. Alijaribu kumpigia rafiki yake lakini hakuwa akipatikana. Frank alihisi labda rafiki yake aliamua kumuuza kiaina. Aliamua kuuliza njia ya kurudi kwao Mbeya na kuanza mdogo mdogo kama utani akiitafuta Chalinze kuelekea kwao.
Ukiachana na ugumu wa safari ya kutembea kwa mguu, lakini pia alikuwa na hasira kwa kuona kuwa rafiki yake amemuuza. Heri angemuacha abaki Mbeya tu japo alikuwa hana kazi. "Sasa ndugu yangu si bora ungeniacha kwetu tu Mbeya kuliko kutesana hivi aisee" Alijisemea moyoni.
Baada ya kuchoka akiwa njiani siku kadhaa aliamua kukaa chini pembezoni mwa barabara na kuamua kulia sana kwa maumivu aliyokuwa anapitia.
Hapo ilikuwa ni katika Vijiji vilivyokuwa katika maeneo ya karibu na mto Ruaha wakati ikiwa hiyo ni siku ya tatu ya safari yake. Kumbuka kuwa jamaa hakuwa na nguo za akiba hivyo nguo alizokuwa nazo zilikuwa zimeshachafuka sana. Waliomuona akipita njiani walimpuuza na kudhani kuwa alikuwa kichaa. Hii ilimpelekea pia kukosa lifti katika magari ambayo aliomba msaada.
Akiwa amesinzia pembezoni mwa barabara, kwambali mbele yake aliona fuso ambalo lilikuwa imebeba mananasi. Gari ile lilikuwa limesimama kwasababu walikuwa wameharibikiwa tairi. Frank aliamua kwenda kuwaelezea shida yake na aombe msaada wamfikishe japo mbele tu kidogo apate kupumzika. Kwa bahati nzuri jamaa walikubali hivyo waliendelea kusaidiana katika harakati za kufungua na kufunga tairi jingine.
Lakini gari ile ilikuwa inaishia iringa tu lakini pia Frenk alishukuru sana kwani watakuwa wamemsogeza kiasi kikubwa cha safari yake.
Alishushwa katika Kijiji cha Ipogolo njiani kuelekea Mbeya na gari ikapandisha njia ya kuelekea Iringa mjini.
Kwakuwa jamaa alikuwa amechoka sana alilala pale stand akijifanya naye ni miongoni mwa wasafiri lakini alikuwa akizuga tu hakuwa msafiri ambaye alikuwa na uhakika wa kupata gari bali alikuwa msafiri wa kutumia miguu yake miwili kwani hakuwa na hela ya kupanda gari. Kulipokucha tena alianza mdogo mdogo na safari yake kuelekea kwao Mbeya.
Tulikuwa na mengi ya kumuuliza Frank kuhusu safari yake hii ya mashaka lakini kutokana na ufinyu wa mda wake alisema "Brother we acha tu safari ilikuwa na changamoto nyingi sana lakini leo tuishie hapo tu" Tulimuomba Fran atusimulie kuhusu rafiki yake, je? alibahatika kumpata tena katika simu?
Frank aliendelea;-
Baada ya kufika Mbeya ndani ya takriban siku sita hivi, alikaa kama wiki tatu na alifanikiwa kumpata lakini rafiki yule alimueleza stori ambayo ilikuwa inahuzunisha zaidi.
Yule bwana kumbe katika harakati za kazi yake kama tulivosema kuwa alikuwa ni dereva wa daladala. Jamaa yule alipata ajali ya kugongana uso kwa uso na gari jingine, katika ajali ile abiria wawili walikufa pamoja na kondakta wake. yeye alijeruhiwa vibaya sana na alipotesa simu na pesa na vitu vingine. Na wakati wote huo alikuwa hospitali baada ya kupoteza fahamu kwa siku nzima. Na wakati huo wanaongea ndio kwanza alikuwa na siku ya pili tangu atoke hospitali.
Kwakweli ule ulikuwa ni mtihani kwa wote wawili Frank na rafiki yake.
Kwa sasa Frank ni dereva wa bajaji hapa Jijini Mbeya. Tulikuta naye tukiwa tumepanda bajaji yake na ndipo alitueleza kisa hiki naye aliridhia kuwa kisa hiki tukiweke katika Stori yetu ya Jumamosi ya leo katika Kipindi chetu cha sitosahau.
Kama utakuwa ulipitwa na visa vilivyotangulia unaweza kuvipata hapa chini
Pia nawe unaweza kushea nasi kwa kutupa kisa chako kupitia mawasiliano yetu ambayo yanapatikana kwa kubofya HAPA
ASANTE NA KWAHERI
Tukutane Jumamosi nyingine panapo Majaaliwa ya ALLAAH
COMMENTS