"Na mwenye kupuuza utajo wangu basi atakuwa na maisha ya dhiki"....
Assalaamu alaykum warahmatullahi wabarakaatuh.
Ninamshukuru Mwenyezimungu kwa kunijaalia afya na uwezo wa kuweka makala hii hapa katika mtandao wa mrbunduki.com
Bila shaka nawe umejaaliwa afya njema, kama ndivyo tunapaswa kumshukuru Mwenyezimungu na kuwaombea wenzetu ambao ni wagonjwa na wale ambao wametangulia akhera.
Leo katika sehemu ya DINI nitawaletea mada tajwa hapo juu, kwani nimeona ni vema kuzinduana juu ya jambo hili.
Allaah anasema katika QUR AN sura ya 20 (surat Twaha) aya ya 124
"Na mwenye kupuuza utajo wangu (Mungu) Basi mtu huyo atakuwa na maisha ya dhiki hapa duniani na atafufuliwa kipofu siku ya Kiyama".....

Leo ningependa tuzungumze kuhusu aya hii na maelezo yake kwa ufupi na jinsi inavyotufanyia kazi leo katika jamii kwa wale ambao ni miongoni mwa tuliouacha utajo wa Allaah.
Kisha baada ya hapo nitasimulia kisa cha kijana mmoja ambaye tumemuomba kwa ridhaa yake tukiweke hapa ili na wengine wajifunze kupitia kisa chake.
Usiache kuacha maoni yako sehemu ya COMMENT na kushea na mwingine elimu hii ili kwa uwezo wa ALLAAH tupate manufaa (Aaaamin)
Mwandaaji / Mwandishi / Mhariri ni mimi mtumishi wako SAIDI RASHIDI BUNDUKI
Nitakwenda kwa mtiririko huu;-
1. Utajo wa MUNGU ni upi?2. Ipi faida ya Utajo wa Mungu?3. Kwanini uwe Utajo wa Mungu na si vinginevyo?4. Ni vipi kuacha utajo wa Mungu?5. Ni yapi maisha ya dhiki hapa duniani?6. Historia fupi ya kijana Hemedi Ally
UFAFANUZI
1. UTAJO WA MUNGU NI UPI?
Katika Quran tukufu tumeamrishwa kuwa tumtaje Mwenyezimungu kwa wingi. Na kumtaja huku kuko katika njia nyingi ambazo zote zinafaa. Lakini katika njia kubwa za kumtaja ALLAH ni Kusoma Quran mara kwa mara kwani haya ni mawasiliano ya moja kwa moja naye.
Lakini ziko adhkari nyingi kama vile
i) Tasbihi (Subhaanallaah)
ii) Tahlili (Laa ilaaha illa llaah)
iii) Tahmid (Alahmdu lillaah)
iv) Takbir (Allaahu akbar)
Lakini pia Allaah ana MAJINA 99 ambayo kwa muislamu ni muhimu kuyajua na kuyasoma mara kwa mara kwani ni kinga na huleta ladha na faraja kwa mwenye kuyatamka.
Hali kadhalika zipo nyiradi nying sana na adhkari nyingi ambazo ni muhimu katika maisha ya kila siku ya muislamu. Na hivi ndivo muislamu hutakiwa kuishi kwa kufuata haya.
2. NI IPI FAIDA YA UTAJO WA MUNGU?
Unaweza ukajiuliza labda ni ipi faida ya kumtaja Mwenyezimungu? Faida ziko nyingi sana lakini kikubwa ni kuwa hayo ndiyo maisha ambayo Mwenyezimungu na mtume wake wameusia tuishi ambayo ndio mafundisho ya Dini ya Uislamu.
Hizi ni chache katika faida nyingi;-
- Kupata radhi kwa Allaah kwa kuishi vile apendavyo yeye
- Kupata amani na faraja katika moyo kutoka kwa Allaah
- Kuwa ni mwenye kuridhika na kile alichokuruzuku Allaah
- Kuwa na amani ya maisha
- Kujiamini katika dunia dhidi ya viumbe wake wazuri na wabaya
- Kuweza kuwa mbali na Sheitwani wa majini na binadamu
- Kukumbuka kesho na kuweza kuiacha dunia (Kuipa mgongo dunia)
- Kuwa kiigizo chema kwa familia na kizazi kilichopo na kijacho
Hizi ni faida chache katika nyingi ambazo atazipata mwenye kudumu na kumtaja Mwenyezimungu mara kwa mara (Kila siku). Mwenyezimungu atujaalie tuwe ni miongoni mwa watu wema (Aamin)
Soma pia makala hii
3. KWANINI UTAJO WA MWENYEZIMUNGU?
Allah ndiye aliyetuumba, na aliyeumba kila kitu. Ametuleta hapa duniani kwa lengo moja tu la kumuabudu yeye na si vinginevyo. Hivyo kumtaja yeye ni miongoni mwa ibada kubwa sana ambazo ametuamrisha kuzifanya.
Lakini pia ametuamrisha kumswalia na kumtakia Rehma Mtume wake Muhammad (S. A W) pamoja na mitume wengine waliotangulia kabla yake.
4. NI VIPI KUACHA UTAJO WA MUNGU?
Hii iko wazi, ni kitendo cha kujisahaulisha na kujiona huna umuhimu wa kutamka nyiradi , kusoma Qur ani, kufanya ibada nyingine na kadhalika. Wengi tunaona kuwa haya ni mambo ya watu maalum peke yako (Mashekhe na Ma ustadh).
Lakini dini imeshuka kwa wote na maamrisho yote na makatazo ni kwa viumbe wote mimi na wewe ndugu yangu unayesoma makala hii.
5. NI YAPI MAISHA YA DHIKI KWA MWENYE KUACHA UTAJO WA ALLAH?
Maisha ya dhiki yamegawanyika katika sehemu nyingi tofauti, lakini ningeomba ufuatane nami katika kisa kifupi cha bwana Hemedi Ally nadhani hapo ndipo tutaona maisha ya dhiki.
Sipendi sana kukuchosha msomaji wangu kwa kusoma makala ndefu saaana, hivyo naomba ufuatane nami kuisubiri sehemu ya pili ya makala hii ili tuendelee kujifunza.
Kwa uwezo wa Allaah tunatarajia kuichapisha kesho mchana. Usisite kuwa nasi
Lakini pia unaweza kusoma hii
Tunaomba radhi kwa pale ambapo tumeteleza kwani hakuna mkamilifu zaidi ya ALLAAH.
WALLAAHU AALAM
(Mungu ndiye mjuzi zaidi)
COMMENTS